Kila siku hazeeki, pamoja na wengi kuamini anakwenda kuchoka lakini Cristiano Ronaldo anaonekana ni yule yule, mwaka juzi, mwaka jana na mwaka huu Cristiano Ronaldo hajabadilika.
Alipofunga penati ya juzi dhidi ya Juventus alivua jezi kama alivyofanya pia mwaka 2014 wakati akiifunga Madrid, Ronaldo anaonekana vile vile mwili umejaa misuli na tumbo lake limekatika katika.
Cristiano anatajwa kama moja ya wachezaji wanaopiga tizi sana duniani, muandishi mmoja nchini Brazil aliwahi kudai kwamba CR7 anapiga push ups 5000 kwa siku jambo ambalo halikufahamika kama kweli au laa.
Lakini ukweli ni kwamba Ronaldo ni mtu wa gym sana na hata baada ya mechi wakati wenzake wakielekea nyumbani kupumzika, yeye hutafuta namna ya kuuweka fiti zaidi mwili wake baada ya mechi.
Baada ya mechi Cristiano Ronaldo huwa anarudi nyumbani kwake, akifika huwa anaogelea sana masaa machache baada ya mpira na huutumia muda huo kwenye swimming pool yeye pamoja na mwanae Ronaldo Jr.
Baada ya kuogelea kinachofuata ni kwenda katika chumba maalum, ambako kunakuwa na maji ya moto sana pamoja na baridi pia kunakuwa na wataalamu wa massage na akimaliza hapo ndio anapumzika.
Cristiano anatajwa pia kuzingatia sana kuhusu ulaji na ndio maana hagusi pombe, anawasisitiza wachezaji wenzake kula protein kila baada tu ya mechi lakini wenzake huwa wakimaliza mechi tu wanaondoka na yeye hula kwanza kabla ya kwenda kuogelea.
Mazoezi ya Ronaldo yameisukuma kampuni ya michezo ya Marekani ya Crunch Fitness kuingia mkataba na CR7 na sasa wako mbioni kujenga Gym 100 ambazo zitakuwa na jina la Cristiano Ronaldo.
Huyo ndio Cristiano Ronaldo, miaka 33 lakini bado anaonekana ana nguvu na bado mwili wake unaonekana kujengeka kama alivyokuwa akiwa na miaka 26, maisha yake yawape funzo vijana wetu na wacheza soka.